連載 Tanzania Leo      by Respicius Shumbusho Damian

トップ ページ 
笑う講座 
カンカン仲間募集 
開店!東アフリカ商店 
漫画DEマサイの美容室 
珍連載 ドドンパ!呪医 
リンク 
[Open Mind Tanzania and Urafiki-blog][Tanzania Leo]

Tanzania Leo

Undani wa Utamaduni wa Mtanzania Kisiasa

Respicius Shumbusho Damian

Toleo la 1: Tulikotoka

Tazania inajulikana sana katika historia kama “Kisiwa cha Amani,” jina amabalo lilitumika kufikisha ujumbe kwamba ni nchi ambayo hakuna wala haitegemewi kuwepo machafuko ya aina yoyote ya machafuko na vurugu za kisiasa, kikabila, kiitikadi au mambo mengine ambayo yangesababisha vita. Jina hili liliifanya Tanzania kutengwa kimtazamo na chi za Africa karibia zote ambazo nyingi zimepitia historia ya vita hasa kuanzia miaka ya 1960 Uhuru wa Afrika. Tanzania ikawa sehemu ya kupumzikia wageni kutoka nchi mbali mbali ambao wengi walikimbia machafuko na ubaguzi wa rangi katika nchi zao. Mwarabu, mzungu, mswahili, mhindi, mchina, na kadharika waliweza kuishi nchi moja na kuifurahia amani japo tukikumbuka hadi miaka ya 1980 katika baadhi ya Miji mikubwa mfano Dar es salaam, Mwanza na mingine ilikuwa ni kitu cha kawaida kutofautisha mitaa kwa kutumia rangi yaani Mtaa mwingine kuitwa Uswahilini (Kwa watu wa hali ya chini), mingine uzunguni (watu wa hali ya juu) na mingine Uhindini au Uarabuni (hii ikiwa ni mitaa ya watu wa hali ya kati wakiwemo waafrika matajiri wa kati).

Uzungu, uhindi, na uswahili haukikua na kusababisha kutofautiana. Hata hivyo mzazi wa taifa tunayemkumbuka kwa jina la baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Raisi wa kwanza wa Tanzania alizidi kuwakuza watoto wake ambao mbali na utofauti wa kipato, makabila, makazi, rangi na mengine mengi, katika imani ya kwamba wao ni wamoja na mshikamano,umoja na kupendana ndiyo misingi ya familia kubwa ya mtanzania. Vile vile hata yule aliyetofautishwa kwa jina la rangi yake mfano mzungu au mwarabu alibakia kuheshimika na kufurahia amani kati ya matunda mengi ya uhuru.

Miaka ya 1980 ambapo nchi nyingi za Afrika zilikuwa katika mgawanyiko wa kiitikadi, baadhi zikifuata na kuamini misingi ya siasa za magharibi (yaani ubepari) zikiongozwa na Marekani, na zile za mashariki(yaani Ujamaa ambao una chembe nyingi za kikomunisti). Kaman chi nyingi zilivyofanya kujitangaza kuamini ujamaa kutokana na makovu ya ukoloni, Tanzania ilijitahidi kujenga ujamaa wa kiafrika ambao ulizidi kusisitiza umoja na haki kwa wote. Katika harakati hii waliokuwa na utajiri mkubwa usiojulikana ulivyopatikana walikosa amani kwa kiasi Fulani,japo hakuna mtu wa kabila moja aliyepigana na kumnyang’anya wa kabila lingine mali yake wala wa rangi moja kufanya hivyo kwa mtu wa rangi nyingine. Neno ‘Umma’lilisaidia kutunza amani. Kila ambaye mali yake ilitaifishwa alimchukia huyo Umma ambaye ilikuwa ni vigumu kumpata.

Mali nyingi na njia kuu za uzalishaji mali zikawa mali ya umma, ambaye wachambuzi wengi wamemlaani kwani machungu yake juu ya mali hizo yalikuwa ni kidogo sana na hivyo kuwaacha wajanja wachache kuendelea kujifaidisha huku wengi wakiendelea kuwa maskini. Nje ya yote haya watanzania waliendelea kuushika usia wa baba Nyerere wa kuilinda amani pamoja na kwamba ilikuja kugeuka nyundo ya kuwakandamiza wanyonge ambao walikuwa wanaona kuwa waliopewa mamlaka kusimamia na kulinda mali ya umma kwa niaba ya wananchi wanajilimbikizia mali wenyewe huku wananchi wakizidi kuteswa na maadui wakuu watatu wa taifa letu. Kimsingi jitihada zote ikiwemo utaifishaji wa njia kuu za uzalishaji mali zililenga kupigana na kuulia mbali hawa maadui wakuu watatu, yaani umaskini, maradhi na ujinga.

Huenda nimlaumu mwalimu aliyefundisha na kuturithisha tamaduni nyingine za taifa letu (kikiwemo kuheshimu na kunyenyekea mamlaka, kuvumilia kupita kiasi, kuipa kipaumbele amani kuliko chochote, kupinga ukabila na pengine woga kwa mwananchi wa kawaida) alishindwa au alisahau kufundisha utamaduni wa kuiweka haki kileleni mwa yote na kuwarithisha viranja wake tamaduni kama vile kuheshimu mali ya umma, kutanguliza maslahi ya taifa kabla ya maslahi binafsi na uchu wa madaraka. Baadhi ya tabia hizi zimekua na kulifanya taifa letu likiwa na viongozi wa aina tatu; Kwanza wapo wale ambao wana njaa kama punda, hata wale usiku kucha hawashibi(humu ndimo ufisadi, rushwa, upendeleo na ufujaji wa mali ya umma wanapatikana). Pili, wapo ambao wananapenda kila mwananchi aendelee na kuufurahia uhuru na utamu kisiwa cha amani lakini wanazidiwa nguvu sana na hawa wenzetu ambao mizizi yao imeenda chini sana kiasi kwamba kuwang’oa ni kazi ngumu.Pia wanaogopa sana hawa wa kundi la kwanza kwani ni rahisi sana kuhatarisha maisha yao mara tu wakionekana wanawazibia mirija yao haramu inayowapatia kipato kisicho halali. Na mwisho wana mtandao mkubwa wa nguvu ya kiuchumi kutoka nje na ndani ya Tanzania, HIVYO ni vigumu kutikiswa.

Kundi la tatu ni la wachapakazi na wapenda maendeleo ya wote, lakini bado tu hawawezi kufanikiwa peke yao kwani wanawahitaji sana hawa wa kundi la kwanza ambao pamoja na ubovu wao wote tuliousikia wana siraha iitwayo uzoefu. Hawa ni kama Waganga wanaotegemewa sana kufanya tambiko siku hadi siku ili serikali yetu iwepo na nchi yetu izidi kuwa na amani (japo mimi imani hii naona siyo ya kweli). Muda mwingine viongozi wetu wazuri wanatambua kuwa tunaweza kuendelea bila kuwa na watu hawa, lakini wanaogopa kuwatia aibu kwani waliheshimiwa tangia taifa letu lipate uhuru. Kwa maana nyingine; wao ni picha ya taifa, uchafu walionao ndani yao ukiwekwa wazi kwa umma na watu kutoka nje watagundua kuwa taifa na serikali yetu ina uchafu uliojificha ndani yake ambao kwa kuwa na macho madogo hawawezi kuuona.

Hivyo inabidi tutambue kabisa kwamba kuna mambo makubwa manne (i) Historia yenyewe imetujenga na tukawa tulivyo hivyo mabadiliko ya historia yenyewe yatazidi kutubadili hadi mwisho wa historia. (ii) Tofauti ni kitu cha kawaida katika jamii yoyote na ndizo huibua kasi ya mabadiliko, hivyo hata zikifichwa kwa muda mrefu kwa njia Fulani mwisha historia yenyewe itaziibua tofauti ili ziweze kuiruhusu historia ya jamii hiyo kuwepo na kupiga hatua. (iii) Lazima jamii au serikali yoyote iwe na mazuri na mabaya; japo walio madarakani hupenda yatangazwe mazuri tu, mwisho wa yote tofauti kati ya viongozi wenye dhamana ya kuiongoza jamii hiyo huzaliwa na historia, na tofauti hizi hubeba chembe za ukweli, kutokubaliana, uwazi na misuguano mingi (hata umwagaji damu). Hii ndiyo huishia katika mabadiliko na kukubaliana kwa muda hadi mabadiliko mengine yajitokeze. (iv)  Tofauti na migogoro hailengi kuvuruga amani; malengo makuu ni kuisahihisha jamii, ila katika masahihisho ya jamii yoyote migogoro, vurugu, uadui na kusutana ni dalili za kawaida.

Basi tofauti ndivyo zilivyoanza kati ya watanzania, hasa hasa miaka ya 1990 ikifuatia mabadiliko yaliyokuwepo ulimwengu mzima. Mabadiliko haya ni pamoja na kukua kwa mawazo ya kimagharibi kama vile Demokrasia, Haki za binadamu, Soko Huria na siasa vya vyama vingi. Mabadiliko haya Tanzania yamekuja kufuatia ulegevu wa misukumo ya siasa za kijamaa kutoka nchi za Ulaya mashariki (hasa Urusi) ambao ulikuwa unayapa mlango mawazo ya kimagharibi ambao kwa wengine wanayatazama kama ukombozi wa fikra.

Naweza kukubali kuwa upepo wa siasa za magharibi umeleta mabadiliko makubwa katika siasa za Tanzania ambazo kwa tangia 1977 zilijengewa imani ya msingi kwamba kuwepo chama kimoja kutasaidia katika kudumisha mshikamano na umoja katika kujenga taifa. Mapema miaka ya 1980 ilikuwa si rahisi kukubalika kuunda mashirika ya kiraia ama vikundi vyovyote ambavyo vingeikosoa serikali ikidhaniwa kwamba ingechangia kuangusha umoja na kutoa nafasi kwa kuzaliwa kwa uasi kwa serikali.

Ni kweli kwamba umoja ulikuwepo, lakini vile vile wajanja wachache walitumia nafasi hiyo kuwanyima haki raia wema kuikosoa serikali na idara zake maana kila jaribio la kuungana kuikosoa serikali lilionekana kama uasi au jaribio la kuleta migawanyiko. Mbali na suala la haki serikali ya Chama Cha Mapinduzi, kwa wengi ilionekana kushika kila nafasi ya maamuzi na kuulinda mfumo na imani za chama badala ya mawazo ya raia. Kwa wengine hadi mwaka 1985 ilikuwa ni vigumu kutofautisha chama na serikali ikiwa ni pamoja na viongozi wa chama kuwashurutisha watendaji wa serikali kutenda si kwa utalamu bali kulinda itikadi na imani ya chama. Ndani ya hali hii miradi yote tuliyoita ya umma hapo awali ilikufa kutokana na usimamizi mbaya.

Hali hii ilipelekea kuvipa nguvu vikundi vya kiraia na kuzaliwa utofautiono wa mawazo na mwisho mfumo wa vyama vingi Tanzania Mwaka 1992. Tangu kuanza kwa mfumo wa siasa ya vyama vingi nchini yapata miaka18 iliyopita, bado uwezo wa vyama kusimama kama vyama kwa maana ya kushika hatamu mbalimbali za uongozi ni mdogo.

Kadiri mfumo huo unavyozidi kupata umri ndivyo msisimko wake unavyoonekana kuzidi kupungua hususani kwa wananchi ambao bila kuvikubali haviwezi kuimarika. Wanaharakati na wafuasi wanaeleza kuwa sababu ni pamoja na; muundo wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, matumizi mabaya ya vyombo vya dola hususani wakati wa uchaguzi na mikutano na mihadhara ya kisiasa ambayo ndio hupaswa kutumika kueneza sera za vyama husika.

Vile vile ikiangaliwa kwa undani kuna ukosefu wa elimu ya uraia miongoni mwa wananchi ambayo ingewafanya watambue umuhimu wa ushiriki wao katika mambo ya siasa, upinzani wa wazi na kuondoa hofu ya kutengwa baada ya kujiunga na vyama vya upinzani. Hivyo vyama vimekuwa vikikosa nguvu tena za kutetea na kusimamia mambo ya msingi ambayo yamekuwa kero kwa wananchi na badala yake kutoa mwanya kwa asasi za kiraia na zisizo za kiserikali, kuwa wakosoaji wa serikali, jambo linaonekana kutoifurahisha serikali siku zilizopita.

Ukweli ni kuwa idadi kubwa ya Watanzania ni wenye elimu ya chini na ndio wanaoongoza katika kujihusisha na masuala mengi ya kisiasa kama kujiandikisha kupiga kura, kuhudhuria mikutano ya siasa pamoja na kushangilia matokeo ya chaguzi. Wanaokubaliana na mfumo wa vyama vingii ni wale ambao wana elimu ya kutosha katika kuchangia maoni ya msingi na sera lakini hukosa ushiriki wa moja kwa moja katika kuunga mkono vyama. Naamini kuwa vyama vina sera nzuri isipokuwa havijajulikani ipasavyo na kuenea kutokana na ukosefu wa uwezo wa kujikimu kiuchumi. Upo umuhimu wa wananchi kuelimishwa kuhusiana na elimu ya uraia ili kutambua umuhimu wa kushiriki katika mambo muhimu ili jukumu libaki kwa wananchi wenyewe kuamua chama cha kukiunga mkono badala ya kuwafanya wauone upinzani kama uasi au ugaidi. Kipindi cha uchaguzi mkuu mwaka 2005 nilikuwa katika jimbo la Karagwe wilayani Karagwe-Mkoa wa Kagera nilichojifunza ni kwamba watu wengi wamejengewa imani kwamba wafuasi wa vyama vya upinzani hawana akili timamu.

Pamoja na dhana potofu iliyostawi Tanzania kuwa nia ya vyama hivi ni upinzani tu katika kila jambo, vimekuwa muhimu katika kuwaamsha viongozi usingizini na kuwahimiza kuongoza kwa haki, uwajibikaji na kuweka maslahi ya wananchi mbele badala ya kuweka mbele maslahi yao binafsi. Naamini kwamba kufa kwa vyama vingi vya siasi kungepelekea utawala wa kidikteta wa chama kimoja ambacho ni wazi kuwa kilizoea kutumia ubabe katika kuamua.

Mpaka sasa tunakubaliana kuwa wabunge wa upinzani humezwa kila wakati linapokuja suala la maamuzi muhimu bungeni. Hili ni kovu la enzi za mfumo wa siasa ya chama kimoja ambapo viongozi waliegemea zaidi katika kulinda maslahi ya chama badala ya maslahi ya wananchi ambao kila kukicha wamekuwa wakiumizwa na makali ya maisha na umasikini.

今日のタンザニア

−タンザニア人の政策文化の内実−

レスピシウス・シュンブショ・ダミアン

 

 

 

日本語訳が入ります。もう少々お待ちください。

Urafiki-Blogで連載中。

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

[トップ ページ][笑う講座][カンカン仲間募集][開店!東アフリカ商店][漫画DEマサイの美容室][珍連載 ドドンパ!呪医][リンク]